Nyoni apewa mikoba ya Morris Stars

Kocha wa Taifa Stars, Kim Poulsen
KOCHA wa Taifa Stars, Kim Poulsen amesema atamwanzisha beki Erasto Nyoni kuziba pengo la Aggrey Morris katika mchezo wa Jumapili dhidi ya Gambia kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Nahodha huyo msaidizi wa Stars, Morris ataikosa mechi hiyo ya Jumapili kwa sababu anatumikia adhabu yake ya kadi nyekundu baada ya kupata kadi mbili za njano katika mchezo dhidi ya Ivory Coast wiki iliyopita ambao pia ulikuwa wa kusaka tiketi ya kushiriki fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika Brazil 2014.

Kim alisema hayo jijini Dar es Salaam baada ya kumalizika kwa mazoezi ya jana asubuhi ya kikosi hicho kwenye Uwanja wa Karume.

“Aggrey (Morris) hatakuwepo kwenye mchezo wa Gambia, anatumikia adhabu ya kadi nyekundu aliyopewa Ivory Coast, lakini nitamwanzisha Nyoni kucheza nafasi yake,” alisema Kim.

“Nilimwona anavyocheza dakika chache kwenye mchezo wa Ivory Coast, alicheza vizuri na kwa utulivu, ni mchezaji mzoefu na anajua jinsi ya kumdhibiti adui.”

Alisema, "hakuna mabadiliko makubwa kwenye kikosi, nafikiri hakutakuwapo na sura mpya zaidi ya wale waliocheza mchezo uliopita na Ivory Coast."

"Nafikiri itawasaidia kuelewana na kucheza kwa mpangilio ulio sahihi, nafahamu kila mmoja wetu anataka kuona tunaifunga Gambia," alisema Kim.

Aliongeza kuwa hana wasiwasi kukosena kwa Morris kwani anawaamini wachezaji wote aliowaita kwenye kikosi hicho kwamba ni wazuri na wenye kucheza nafasi zaidi ya moja uwanjani.

“Kila namba nilijaribu kuita wachezaji wawili, nilifahamu inaweza kutokea mmoja ameumia au kutumikia adhabu ya kadi, nafikiri yote yametukuta, lakini tunasonga mbele," alisisitiza Kim.

Kocha huyo amemwondoa kwenye kikosi hicho beki wa Simba, Masoud Nassoro 'Chollo' kutokana na kuumia goti.

Daktari wa timu hiyo Mwanandi Mwankemwa alisema, "uchunguzi unaonyesha tatizo hilo ni la muda mrefu kwa Chollo, alijitonyesha, atachukua muda kidogo kurudi katika hali yake ya kawaida."

Wachezaji wengine ambao walikuwa majeruhi, lakini wamejiunga na wenzao na kufanya mazoezi ni viungo, Haruna Moshi 'Boban' na Nurdin Bakari.

Wakati huohuo; mtaalamu wa tiba ya viungo wa klabu ya Azam FC, Paulo Gomez amejitolea kuwafanyisha mazoezi maalumu Haruna Boban' na Nurdin ili warejee kwenye kikosi cha Stars haraka.

Boban, Bakari, Said Nassoro 'Cholo'na Thomas Ulimwengu  hawakujumuishwa kwenye kikosi cha Taifa Stars kilichoikabili Ivory Coast ugenini kutokana na kusumbuliwa na majeruhi.

Mmoja wa viongozi wa bechi la ufundi la Taifa Stars aliliambia Mwananchi kuwa Gomez pia ndiye alichunguza afya za wachezaji wote wa timu hiyo siku mmoja kabla ya safari ya Ivory Coast na kubaini matatizo kwa Boban na Cholo yaliyosababisha  kuondolewa kwao.

Akizungumza na Mwananchi mara baada ya kumaliza programu yake ya mazoezi na wachezaji hao kwenye Uwanja wa Karume, Gomez alisema anafanya kazi hiyo bila malipo yoyote kutokana na mapenzi yake kwa Tanzania.

"Mimi ni mtaalamu wa tiba za viungo, TFF iliniomba nije niwasaidie na mimi nilikubali kwa moyo mmoja.

"Hapa nilipo najitolea tu silipwi chochote na mimi naridhika kwa sababu napenda kuisaidia Tanzania,"alisema Gomez.

Gomez alisema kuwa mazoezi anayowapa Boban na Bakar yana lengo ya kumaliza maumivu na kuwarejesha katika hali ya kawaida.

"Mazoezi haya yanachukua dakika 45 mpaka saa moja, ni aina ya mazoezi ambayo lengo lake ni  kumwezesha majeruhi kurejea katika hali ya kawaida,"alisema Gomez.  source: mwananchi.co.tz

0 comments

Leave a Reply