LLYOD NCHUNGA ajiuzulu uenyekiti Yanga

Image

MWENYEKITI wa Yanga, Lloyd Nchunga ametangaza kujiuzulu wadhifa huo kuanzia jana.

Kujiuzulu kwa Nchunga itakuwa furaha kwa Baraza la Wazee la Yanga, ambalo karibu mwezi mzima sasa limekuwa likimshikia bango Nchunga aachie madaraka kwa madai ya timu hiyo kufanya vibaya katika Ligi Kuu Tanzania Bara iliyomalizika mapema mwezi huu, ambapo Yanga ilishika nafasi ya tatu.

Pia itakuwa imewarahisishia kazi baadhi ya wanachama wa Yanga, ambao walikutana makao makuu ya klabu hiyo makutano ya mitaa ya Twiga na Jangwani na kutangaza kumpindua Nchunga, uamuzi ambao ulipingwa na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kwamba ni kinyume cha Katiba.

Uamuzi huo wa Nchunga kujiuzulu aliutangaza jana kwenye mkutano wake na waandishi wa habari uliofanyika ofisini kwake jengo la NSSF, Dar es Salaam na kwamba amefanya hivyo kwa maslahi ya Yanga.

Alisema uamuzi wake wa kujiuzulu umekuja wakati walishakubaliana kwenye kikao cha
Kamati ya Utendaji ya Yanga kwamba wajumbe wengine waliobaki wasijiuzulu hadi mkutano mkuu wa wanachama Julai 15 mwaka huu, lakini mazingira yamemfanya afikie uamuzi huo na kwamba anajua wenzake watasononeka sana.
more information; http://www.habarileo.co.tz/michezo

0 comments

Leave a Reply